WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya
juzi alilazimika kuweka mambo sawa juu ya usahihi wa ziara za Rais
Jakaya Kikwete nje ya nchi.
Profesa Mark Mwandosya alilazimika kusimama bungeni ili kutuliza
upepo, kutokana na hatua ya baadhi ya wabunge wa kambi ya upinzani
bungeni kupotosha kuhusu ziara hizo za Rais, walipokuwa wakichangia
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2015/16.
Akikaimu nafasi ya Waziri Mkuu, baada ya Mizengo Pinda kuwa na kazi
nyingine nje ya Bunge, Profesa Mwandosya aliwaambia wabunge kwamba Rais
haendi nje kuomba, bali anatengeneza uhusiano imara wa kidiplomasia,
hatua inayowafanya wawekezaji kuja kuwekeza nchini.
“Rais haendi katika mataifa hayo kama omba omba kama mnavyopotosha
nyie. Anakwenda kuvutia uwekezaji na fedha zinazotolewa hatupewi bure
bali ni mkopo. Hata hili bomba la gesi kutoka Mtwara kuja Kinyerezi, Dar
es Salaam ni mkopo na ni matokeo ya ziara za Rais,” alisema Profesa
Mwandosya.
Katika hatua nyingine, Waziri huyo mwenye ushawishi mkubwa, aliwataka
wabunge wote bila kujali itikadi zao za kisiasa, kuisaidia Serikali
katika kuboresha Mpango wa Maendeleo wa Taifa, badala ya kutumia muda
mwingi kuukosoa bila kutoa suluhisho.
“Nimegundua wabunge wengi mnasimama na kukosoa bila kuboresha Mpango
wenyewe. Hii itawafanya wataalamu wetu kutoka Tume ya Taifa ya Mipango
wanaosubiri michango yenu, kushindwa kupata mambo muhimu ya kuboresha
Mpango,” alisema Profesa Mwandosya.
Alisema hakuna sababu ya wabunge wanaoaminiwa na wananchi katika
kuboresha maisha yao, kutoka nje ya mada ya Mapendekezo ya Mpango wa
Taifa wa Maendeleo na kuanza kujadili mambo ambayo hayana maslahi kwa
taifa.
“Tusiruhusu hisia zetu kutuendesha wakati huu ambapo tunajadili suala
ambalo linagusa mustakabali wa Taifa na wananchi wetu,” alisema Profesa
Mwandosya aliyekuwa akipigiwa makofi na wabunge wa pande zote.
Wabunge wataendelea kujadili Mapendekezo ya Mpango huo wa Maendeleo
ya Taifa uliowasilishwa bungeni na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,
Uhusiano na Uratibu, Stephen Wasira, Jumatano.



0 comments:
Post a Comment