MAELFU ya watu walijitokeza jana kumzika aliyekuwa mwanamuziki mahiri
wa muziki wa dansi nchini, Khamis Kayumbu maarufu Amigolas katika
makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam.
Walikuwapo wasanii wa muziki, maigizo, wasanii wa zamani, wa sasa
pamoja na makundi mbalimbali ya muzi ki. Mwili wa mwanamuziki huyo
ambaye hadi mauti yanamkuta alikuwa kiongozi wa bendi ya Ruvu Stars
inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), alipumzishwa kwenye
nyumba yake ya milele saa tisa alasiri.
Mwanamuziki huyo aliyewahi pia kutamba na bendi ya Twanga Pepeta
akiwa mmoja kati ya waanzilishi wake, alifariki juzi katika Hospitali ya
Taifa ya Muhimbili alipokuwa amelazwa.
Alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya moyo alichangia kwa kiasi kikubwa
mabadiliko ya muziki wa dansi nchini. Alikuwa mahiri zaidi wa kucheza,
kuimba, kutawala jukwaa pamoja na kuchombeza vionjo mbalimbali vya
muziki.
Wanamuziki mbalimbali walimzungumzia mwanamuziki huyo kwa kusema kuwa
alikuwa ni chachu ya maendeleo ya sanaa kwa kuwa alikuwa hana majivuno
na alikuwa akiwasaidia wasanii wengi.
Mwanamuziki Robert Hega maarufu kama Katapila, alisema Amigolas
alikuwa na maisha mazuri kwa wasanii wenzake hata nje ya kazi yake ya
muziki.
Alisema alikuwa akishiriki katika kutoa mawazo ya kuendeleza muziki hata kwa wasanii wasiokuwa kwenye bendi aliyokuwapo.
“Huyu kwangu binafsi nilifanya naye kazi pale Twanga akiwa kama kaka
yangu na alikuwa anajua muziki vyema kuliko hata ambavyo ilikuwa
ikifahamika, lakini hakuwa na nyodo kabisa,” alisema Katapila.
Mwanamuziki mwingine, Muumini Mwinjuma alisema Amigolas alimshauri
mengi na kumtia moyo kuhusu muziki. Moja kati ya nyimbo alizotunga
mwanamuziki huyo ni Aminata alioimba akiwa na Twanga Pepeta.
Katika hatua nyingine, Rais Jakaya Kikwete amemtumia salamu za
rambirambi Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk Fenella
Mukangara kuomboleza kifo cha Amigolas.
“Nimehuzunishwa na kusikitishwa na taarifa za kifo cha mwanamuziki
Khamisi Kayumbu kilichotokea tarehe 9 Novemba, 2014 katika Hospitali ya
Taifa ya Muhimbili (MNH) alikokuwa amelazwa kwa matibabu ya ugonjwa wa
moyo,” alisema Rais Kikwete katika salamu zake
.
Rais Kikwete alisema anatambua mchango mkubwa wa Amigolas, katika
kuhamasisha maendeleo ya nchi kupitia sanaa ya muziki katika
kuwafikishia wananchi ujumbe muhimu wa masuala mbalimbali ya kijamii na
kiuchumi.
Amesema Kayumbu alikuwa mfano unaofaa kuigwa na wasanii wengine kote nchini.
“Kutokana na msiba huu, naomba upokee salamu zangu za rambirambi kwa
kumpoteza mmoja wa wanamuziki mahiri hapa nchini, na rambirambi hizi
ziwafikie pia wanamuziki wengine kote nchini kwa kumpoteza mwenzao,”
alisema.



0 comments:
Post a Comment