Ofisa Afya wa Halmashauri ya Manispaa Morogoro, Gabriel Malisa
amesema halmashauri hiyo ina kata tano zenye wakazi wasio na vyoo,
ambayo ni sawa na asilimia 13 ya wakazi wote wa manispaa hiyo.
Akizungumza ofisini kwake jana, Malisa alisema kuna kampeni maalumu
inaendelea ili kukomesha tatizo hilo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha
elimu inawafikia wakazi hao ili wajenge vyoo bora.
Alitaja kata hizo kuwa ni Kingorwila, Mzinga, Kauzeni, Bigwa na
Mindu. Alisema kuwa mkakati uliopo ni kuhakikisha wakazi hao wanajenga
vyoo ili kusaidia kuondokana na magonjwa ya kuambukiza.
Malisa alisema kuwa takwimu zinaonesha kuwa hapa nchini ni asilimia
22 tu za kaya za mijini, ndizo zenye vyoo bora. Alisema kuwa katika
maeneo ya vijijini ni asilimia 9 tu ya wakazi walio na vyoo bora.
Alisema Manispaa hiyo itakuwa mwenyeji wa siku ya kunawa mikono na
usafi wa mazingira kitaifa kuanzia Novemba 14 na kilele chake ni Novemba
19. Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni “Choo bora na mikono safi kwa afya
bora, utu na usawa.”



0 comments:
Post a Comment